Have you got a good story?

Share your story, discuss the issues with Dailynews Blog.

Have you got a good story?

Share your story, discuss the issues with Dailynews Blog.





Nafasi Ya Matangazo

Friday 30 June 2017

MEGAWATI 5,000 KUPATIKANA 2021 MRADI WA STIEGLERS GORGE WA RUFIJI UKIKAMILIKA

SERIKALI imesema hadi ifikapo mwaka 2021 umeme wa uhakika wa megawati 5,000 utaanza kupatikana nchini baada ya kukamilika kwa mradi wa kuzalisha umeme kwa kutumia  nguvu za maji katika maporomoko ya maji ya Mto Rufiji. Anaandika  Greyson Mwase, wa WNM- Rufiji.

Naibu Waziri wa Nishati na Madini Dk. Medard Kalemani amesema umeme huo utazalishwa katika emneo la Stiegler’s Gorge  lililopo  Rufiji mkoani Pwani ambao utaongeza umeme wa kiasi cha Megawati 2100 katika  gridi ya taifa.


Dk. Kalemani aliyasema hayo Juni 29, mwaka huu katika ziara ya Waziri wa Maji, Nishati na Umwagiliaji kutoka  Ethiopia, Dk. Seleshi Bekele aliyeambatana na wataalam wa masuala ya ujenzi wa mitambo  ya kuzalisha umeme kwa kutumia maji kutoka  Ethiopia kwenye eneo  la mradi wa kuzalisha umeme kwa kutumia maporomoko ya maji ya Mto Rufiji ya Stieglers Gorge wilyani  Rufiji mkoani Pwani.

Dk Kalemani alisema kuwa kupatikana kwa umeme wa uhakika ifikapo mwaka 2021 kutachochea ongezeko la viwanda hivyo kuongezeka kwa fursa za ajira na biashara na kukuza uchumi wa nchi.

Alisema mradi huo mkubwa ni moja ya mikakati ya Serikali  kuhakikisha nishati inakuwa na mchango mkubwa katika  kufikia malengo  ya  Dira ya Maendeleo ya Taifa yenye lengo la kuhakikisha kuwa nchi inatoka katika orodha ya nchi maskini duniani na kuingia katika orodha ya nchi zenye uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025.


Alisisitiza kuwa mbali na mradi huo mkubwa, serikali imeweka mikakati ya kutumia vyanzo vingine vya nishati kama vile Gesi, Makaa ya Mawe, Jotoardhi, Upepo ili kuhakikisha kuwa nchi inapata umeme wa uhakika.


Akielezea mafanikio ya mradi huo mbali na upatikanaji wa umeme wa uhakika, Dk. Kalemani alisema kuwa mradi huo utachochea ukuaji wa shughuli za uvuvi katika mkoa wa Pwani.


Alitaja mafanikio mengine kuwa ni pamoja na kukuza sekta ya Utalii katika  mkoa wa Pwani pamoja na kuzuia mafuriko ambayo yamekuwa yakitokea mara kwa mara katika mto Rufiji na kuathiri makazi  ya wakazi waishio pembezoni na mto huo.


Akielezea hatua iliyofikiwa ya maandalizi ya ujenzi wa mradi huo mkubwa, Dk. Kalemani alisema baada ya timu ya wataalam kutoka Tanzania na Ethiopia kufanya ziara katika eneo la mradi hatua inayofuatia ni wataalam kukaa vikao mbalimbali kujadili namna bora ya kutekeleza mradi pamoja na kubadilishana uzoefu.


Alisema mara baada ya ujenzi wa mradi huo kukamilika, moja ya kazi zitakazofanywa ni pamoja na ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme hadi Chalinze yenye urefu wa kilomita 200 na njia ya kusafirisha umeme kutoka  eneo la Mradi hadi  Singida yenye urefu wa kilometa 800.


Waziri Kalemani aliwataka wananchi na taasisi mbalimbali kuunga mkono  juhudi za Serikali  ya Awamu ya Tano  ikiwa ni pamoja na kulinda vyanzo vya maji  hususan katika mto Rufiji.

Wakati huohuo, katika  ziara hiyo Waziri wa Maji, Nishati na Umwagiliaji kutoka  Ethiopia, Dk. Seleshi Bekele alisema kuwa mradi huu mkubwa ni mzuri na unatekelezeka na kuongeza kuwa  Ethiopia ipo tayari kutoa ushirikiano mkubwa kupitia wataalam wake lengo likiwa ni kuhakikisha kuwa mradi unafanikiwa na kukamilika kwa wakati.

Naibu Waziri wa Nishati na Madini Dk. Medard Kalemani akishuka kwenye helikopta, mara bada ya kuwasili katika uwanja mdogo wa  Stieglers Gorge, Rufiji mkoani Pwani kabla ya kuanza kwa ziara ya Waziri wa Maji, Nishati na Umwagiliaji kutoka  Ethiopia, Dk. Seleshi Bekele aliyeambatana na wataalam wa masuala ya ujenzi wa mitambo  ya kuzalisha umeme kwa kutumia maji kutoka  Ethiopia pamoja na wataalam wa masuala ya  umeme na ujenzi wa mabwawa kutoka Tanzania


Waziri wa Maji, Nishati na Umwagiliaji kutoka  Ethiopia, Dk. Seleshi Bekele (kushoto) akieleza jambo kwa Mhaidrolojia Mwandamizi kutoka Shirika la Umeme  Tanzania (TANESCO), Stanislaus Kizzy (kulia) katika ziara hiyo. Anayesikiliza katikati ni Naibu Waziri wa Nishati na Madini Dk. Medard Kalemani.


Kaimu Kamishna wa Nishati na Masuala ya Petroli, Mhandisi Innocent Luoga (kushoto) akielezea maandalizi ya mradi wa kuzalisha umeme kwa kutumia nguvu za maji wa Stieglers Gorge kwa Mtendaji Mkuu wa kampuni ya Ethiopian Construction Design and  Supervision kutoka  Ethiopia,  Dk. Negede Kassa (kulia) katika ziara hiyo.





Naibu Waziri wa Nishati na Madini Dk. Medard Kalemani akishuka kwenye  boti kwa ajili ya kuelekea kwenye eneo la Stieglers Gorge kutakapojengwa mradi huo.

 Waziri wa Maji, Nishati na Umwagiliaji kutoka  Ethiopia, Dk. Sileshi Bekele ( wa  tatu kushoto) akieleza jambo katika ziara hiyo.


Waziri wa Maji, Nishati na Umwagiliaji kutoka  Ethiopia, Dk. Seleshi Bekele (wa saba kulia) na Naibu Waziri wa Nishati na Madini Dk. Medard Kalemani (wa nane kulia) wakiwa katika picha ya  pamoja na timu ya wataalam kutoka  Tanzania na Ethiopia katika ziara hiyo.


Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Post a Comment