Have you got a good story?

Share your story, discuss the issues with Dailynews Blog.

Have you got a good story?

Share your story, discuss the issues with Dailynews Blog.





Nafasi Ya Matangazo

Sunday 30 April 2017

MPIGAPICHA WA TSN MOHAMED MAMBO ATWAA TUZO YA MPIGAPICHA BORA EJAT 2016

Mpigapicha Mkuu wa Magazeti ya Daily News, Habarileo na Spotileo, Mohamed Mambo akikabidhiwa tuzo ya EJAT baada ya Kuibuka Mpigapicha Bora wa EJAT 2017. Mambo alikabidhiwa tuzo hiyo na Mkurugenzi Mtendaji wa Zamani wa Magazeti ya The Guardian Ltd ambaye pia ni Mkufunzio wa Uandishi wa Habari nchini, Kiondo Mshana katika Hafla ya kukabidhi tuzo hizo jijini Dar es Salaam usiku wa kuamkia leo jijini Dar es Salaam.
**************
Na Katuma Masamba

MPIGA Picha wa Magazeti ya Serikali (TSN), Mohammed Mambo ameibuka mshindi wa tuzo ya mpigapicha bora, huku mwandishi wa gazeti la Habarileo Shadrack Sagati akiibuka mshindi wa pili katika kipengele cha uandishi wa habari za data katika Tuzo za Umahiri wa uandishi wa Habari (EJAT) mwaka 2016.


Hafla ya utoaji wa tuzo hizo ilifanyika jijini Dar es Salaam na ilihusisha vipengele 19 vilivyoshindaniwa na waandishi kutoka kwenye magazeti, radio na televisheni. Jumla ya waandishi 66 waliteuliwa kuwania tuzo hizo zinazoendeshwa na Baraza la Habari (MCT).


Washindi wa tuzo za mwaka huu waliteuliwa na majaji mbalimbali ambao ni Ndimbara Tegambwage, Hassan Mhelela, Pili Mtambalike, Dk Mzuri Issa Ali, Mwanzo Milinga, Nathan Mpangala na Dk Joyce Bazira ambaye alikuwa katibu wa jopo na Valeria Msoka ambaye alikuwa kiongozi wa jopo hilo la majaji.


Kazi zilizowasilishwa MCT kwa ajili ya kushindanishwa zilikuwa zaidi ya  810, zikiwemo zaidi ya 435 kutoka vyombo vya habari vya kielektorini na kazi zaidi ya 374 kutoka kwenye magazeti. Kazi hizo ni nyingi ikilinganisha na zile za mwaka 2015 ambako jumla ya kazi zilikuwa 568. Mshindi wa jumla wa tuzo hiyo kwa mwaka huu ni Florence Majani kutoka gazeti la Mwananchi.


Akizungumza katika hafla ya utoaji wa tuzo hizo hizo, Mgeni rasmi katika hafla hiyo, Jenerali Ulimwengu ambaye pia ni mwandishi mkongwe licha ya kuwapongeza washindi aliwataka waandishi ambao hawakufanikiwa kupata tuzo kuongeza juhudi katika kazi zao.


"Nashauri mkadurufu kazi za washindi, mkaone mlijikwaa wapi na kipindi kingine mtafanya vizuri zaidi," alisema mwandishi huyo mkongwe ambaye alitumia hotuba yake kama kuwafunda waandishi wa habari.


Alisema tasnia ya habari si ya watu walioshindwa masomo na kuikimbilia wakidhani ni nyepesi, bali ni taaluma inayohitaji watu mahiri na makini ambao wamejitolea kufanya mambo yasiyowahusu.


Alisema tasnia ya habari ni muhimu katika maisha ya binadamu kwa sababu inatoa nafasi kwa wanajamii kuungana, kuwasiliana na kubadilishana mawazo ili kuondoa tofauti miongoni mwao kupitia vyombo vya habari.


“… Uandishi wa habari ni shughuli yenye uwerevu na umakini wa hali ya juu wa kujua kitu na matokeo ambayo wanajamii hawana nia, hawajui na hawafahamu. Kuna muda huwa nasema mwandishi wa habari ni yule mtu anayeejiingiza katika mambo ambayo binafsi hayamuhusu, bali yanaigusa jamii,” alisema Ulimwengu.


Ulimwengu aliwataka wanahabari kujituma na kuwa makini katika uandaaji wa habari na kutambua kuwa wanaofanyia kazi baadhi yao wanajua kuliko wao na pia  kutotumia kigezo cha kuwa katika tasnia hiyo kudhani wanajua kuliko wao.


Aidha, alitoa mwito kwa wanahabari nchini kujenga utamaduni wa kujiendeleza kielimu, lakini pia kuwa kujenga tabia ya kusoma mara kwa mara vitabu na majarida, kusikiliza na kujifunza mambo mbalimbali ili waweze kufanikiwa na kutekeleza kazi zao kwa ufanisi.


Alisema mwandishi wa habari asiyependa kusoma vitabu na kujifunza kila wakati hawezi kuwa mahiri na wala kazi zake haziwezi kuwa nzuri.


“Kitabu ni rafiki mkubwa sana kwa wanahabari na hiyo ni silaha, waandishi tunatakiwa kusoma, kusikiliza na kujifunza kwa wenzetu waliofanikiwa. Chukulieni kazi mnayoifanya kuwa ni shughuli muhimu na inayohitaji umakini wa hali ya juu kwani utoa matokeo na kuhabarisha mambo ambayo wananchi hawajui na hawafahamu,” alisema.


Ulimwengu pia alishauri serikali kulinda usalama wa wanahabari kwani hivi karibuni kumeokea matukio ya wanahabari kupigwa na kunyanyaswa wakati wakitekeleza kazi zao.


Aidha, Aliwataka waandishi kuhakikisha wanaweka kumbukumbu sahihi za wanausalama na askari polisi waliowashambulia na baadae kuwadai fedha nyingi kama fidia ya matukio mabaya waliyowafanyia.


“Waandishi mkishambuliwa na hao watu nendeni mahakamani na ukishindwa kata rufaa na huko ndio utaenda kudai fidia kwa kitendo walichokifanyia,” alisema.



Baadhi ya vipengele hivyo ni mwandishi bora wa habari za uchumi, biashara na fedha, habari za michezo na utamaduni, habari za afya, Kilimo, Elimu, habari za uchambuzi wa matukio, habari za utalii.


Vingine ni mwandishi bora wa habari za Afya ya uzazi kwa vijana, habari za Ukusanyaji kodi, habari za uchunguzi, habari za takwimu, Mpiga picha bora, Mchoraji bora wa vibonzo, mpiga picha bora wa televisheni.


RAIS MAGUFULI ATAKA TAKUKURU KUCHUNGUZA UHALALI WA MKATABA WA MANISPAA NA WAKALA WA MAEGESHO MOSHI



 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiongea na viongozi wa dini wa mkoa wa Kilimanjaro baada ya kupata nao chakula cha mchana katika Ikulu ndogo mjini Moshi leo Aprili 30, 2017
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, leo tarehe 30 Aprili 2017, amekutana na kuzungumza na viongozi wa dini wa madhehebu mbalimbali na kuuagiza viongozi wa mkoa wa Kilimanjaro kutatua kero zinazowakabili wananchi wa mkoa huo.

Rais Magufuli ametoa agizo hilo kufuatia malalamiko ya baadhi ya viongozi wa dini kueleza kero zinazowakabili ikiwa ni pamoja na manyanyaso yanayofanyiwa na wafanyakazi wa Wakala wa Maegesho ya magari mkoani humo.

Kufuatia malalamiko hayo, Rais Magufuli amemuagiza Kamanda wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini TAKUKURU kuchunguza mkataba uliongiwa kati ya Manispaa ya Moshi na Wakala wa Maegesho ya magari mkoni humo ili kujua uhalali wake kwani kumekuwa na ubadhirifu mkubwa wa upotevu wa mapato yatokanayo na makusanyo ya maegesho hayo.

'' Uangalie ule mkataba wa parking wa hapa Moshi,kama kuna ufisadi wowote peleka Mahakamani,lakini haya ya administration kayaangalie wasinyanyase watu, huwezi hata ukamuona sheikh unafunga gari lake,ukimuona Mchungaji na kola yake unafunga tu ni ushetani,sasa saa nyingine wale vijana wanaofanya ile kazi wanajisahau, hawaheshimu utu wa Watanzania'' amesema Rais Magufuli.  

Pia amemuagiza Mkurugenzi wa Manisapaa ya Moshi kutoa kibali cha Ujenzi wa Kituo cha Uchunguzi wa maradhi kilichoombwa na mwananchi mmoja mkoani humo ili aweze kuendelea na ujenzi huo kutokana na kutopewa kibali hicho kwa muda mrefu.

Katika hatua nyingine, Rais Magufuli amesema kutokana na Serikali kuzuia unywaji wa pombe aina ya viroba idadi ya vifo katika mkoa wa Pwani imepungua kutoka 80 hadi 20 na hata ajali za pikipiki maarufu Bodaboda nazo zimepungua nchini.


Aidha, Rais Magufuli ametaka uongozi wa Wilaya ya Hai kufanya kazi bila kutishwa na madiwani ikiwa ni pamoja na kubadili sheria ndogondogo wilayani humo ili kupunguza kero za utitiri wa ushuru kwa wananchi.

 Rais Magufuli ametoa maagizo hayo wakati alipokutana na viongozi wa dini wa mkoa wa Kilimanjaro, Vyama vya Siasa na watendaji wa Serikali mkoani humo na kula nao chakula cha mchana kilichoandaliwa na mkoa wa Kilimanjaro.


WAZIRI MAGHEMBE AZIPA HADHI HOTEL ZA DAR ES SALAAM

Waziri wa Maliasili na Utalii Prof. Jumanne Maghembe akizungumza kabla ya kukabidhi vyeti vya kutambua hadhi za Hotel zilizopo jijini Dar es Salaam na kwa kuzipa madaraja mpaka nyota tano katika sokola utali hapa nchini
Waziri wa Maliasili na Utalii Prof. Jumanne Maghembe akikabidhi cheti kwa Meneja Masoko na Mauzo wa Serena Hoteli,Seraphin Lusala mara baada ya Hoteli hiyo kutambuliwa kuwa na hadhi ya Nyota tano katika mkoa wa Dar es Salaam, katika hafla fupi iliyoandaliwa na Wizaraya Maliasili na Utalii katika ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa Mwalimu Nyerere jijini Dar es Salaam
Majaji ambao waliokuwa wakitoa maksi ya hadhi za hoteli hapa nchini wakisimama kujitambulisha kwa wageni waliofika

Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Meja Generali Gaudence Milanzi akizungumza na Wamiliki wa Mhoteli jijini Dar es Salaam leo kabla ya kukabidhi vyeti vya madaraja ya hotel zao

Afisa utalii kutoka bodi ya Utalii Tanzania (TTB),Irene Mville akitoa maelekezo kwa wadau wa mahoteli ambao walifika katika hafla ya ugawaji wa madarajana viwango katika Hoteli zilizopo jijini Dar es Salaam 
Waziri wa Maliasili na Utalii Prof. Jumanne Maghembe akiwa katika picha ya pamoja na wamiliki wa Hotel jijini Dar es Salaam


RAIS DKT. MGUFULI APATA CHAKULA CHA MCHANA NA VIONGOZI WA DINI WA MKOA WA KILIMANJARO

 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiongea na viongozi wa dini wa mkoa wa Kilimanjaro baada ya kupata nao chakula cha mchana katika Ikulu ndogo mjini Moshi leo Aprili 30, 2017
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiagana na viongozi wa dini wa mkoa wa Kilimanjaro baada ya kupata nao chakula cha mchana katika Ikulu ndogo mjini Moshi leo Aprili 30, 2017
Viongozi wa dini wa mkoa wa Kilimanjaro  wakiwa  katika Ikulu ndogo mjini Moshi kupata chakula cha mchana walipata wasaa kueleza changamoto zao mbalimbali kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiongea na  leo Aprili 30, 2017


TIMU YA VIONGOZI WA SERIKALI YAFANYA MAZOEZI YA MWISHO TAYARI KUIKABILI TIMU YA VIONGOZI WA DINI KESHO

 Kocha Mchezaji wa Timu ya Viongozi wa Mkoa wa Mbeya na Mkuu wa Mkoa wa Mbeya,Amos Makalla akifundisha kwa kutumia chati maalum ya kufundishia kwa wachezahi wake.
 Kocha Mchezaji wa Timu ya Viongozi wa Mkoa wa Mbeya na Mkuu wa Mkoa wa Mbeya,Amos  Makalla akitoa maelezo kwa wachezahi wake.
 Mazoezi ya viungo yakiendelea
KIKOSI cha timu ya mpira wa miguu cha mkoa wa Mbeya kibachojinoa kwa mchezo dhidi ya viongozi wa dini leo kimefanya mazoezi yake ya mwisho kabla ya mchezo utakaofanyika kesho katika dimba la Sokoine jijini Mbeya.

Chini ya Kocha Mchezaji wa timu hiyo ambaye pia ndie Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Amos Makalla, timu hiyo ilifanya mazoezi katika uwanja wa Magereza jijini Mbeya.

Akizungumza baada ya mazoezi hayo, Makalla alisema timu yake imejipanga vyema kulipiza kisasi katika mchezo huo ambapo mshindi atakabidhiwa Kombe la Amani 2017.

Makalla pia amewataka wananchi kujitokeza kwa wingi katika dimba la Sokoine kushuhudia mpambano huo wa ainayake  utakao kutanisha viongozi wa mkoa wa Mbeya na Viongozi wa Dini.

"Mechi ni kesho saa 10 :00 jioni uwanja wa Sokoine, jijini Mbeya na Kiingilio ni bure,"alisema Makalla.


Saturday 29 April 2017

NEMC YAZIPIGA FAINI TOMMY DIARIES FARM NA NDOTO FARM MILIONI 20



Mwanasheria wa NEMC Benard Kongola (kulia) akiandika maelezo ya bw Athanas Mushi meneja wa shamba la Tommy Diaries Farm.
 **********
Baraza la Taifa la Hifadhi ya Mazingira (NEMC) limeyatoza faini mashamba ya mifugo ya Tommy na Ndoto jumla ya shilingi milioni 20 kutokana na kukiuka Sheria ya Mazingira ya mwaka 2004.

Faini hizo zilitangazwa na wakili wa serikali mkuu kutoka NEMC, Benard Kongola baada ya kikosi kazi namba tatu cha kunusuru ikolojia ya mto Ruaha mkuu kukagua hali ya uhifadhi wa mazingira katika mashamba ya mifugo ya Tommy na Ndoto yaliyopo wilayani Kilolo Mkoani Iringa jana. 

Baada ya kitamka faini hizo, wakili Kongola alisema kuwa Shamba la mifugo la Tommy limetozwa faini kutokana na kulima mahindi na migomba ndani ya mita 60 kutoka ukingo wa mto Ruaha mdogo. Alisema kuwa shamba la mifugo la Ndoto limetozwa faini kutokana na kufanya biashara bila kuwa na cheti ya tathmini ya hali ya mazingira kutoka NEMC.  

Wakili Kongola alisema kuwa faini hizo zinatakiwa kuwa zimelipwa ndani ya siku 14 toka tarehe ya faini hiyo. Aliongeza kuwa baada ya siku 14 NEMC wataenda kukagua utekelezaji wa agizo hilo.

Kikosi kazi hicho kikiwa katika ukaguzi wa hali ya uharibifu wa mazingira katika shamba la mifugo la Tommy kilibaini uharibifu wa mazingira ikiwa ni pamoja na kupandwa miti isiyo rafiki kwa mazingira na kusababisha kukauka kwa vyanzo vya maji. 

Mwenyekiti wa kikosi kazi hicho ambaye pia ni Katibu Tawala mkoa wa Iringa, Wamoja Ayubu alisema “chanzo hiki cha maji ambacho kinaelekea kukauka lazima kihifadhiwe ili kirudie hali yake ya awali. Miti hii yote ambayo si rafiki kwa mazingira lazima ikatwe na kupandwa miti ambayo ni rafiki kwa maji na niletewe taarifa ya utekelezaji ndani ya wiki moja, alisema Ayubu”.


MAKAMU WA RAIS AZINDUA MRADI WA MAJI UTAKAOHUDUMIWA WILAYA SABA MKOANI TABORA

Makamu wa Rais , Samia Suluhu Hassan akikata utepe kuzindua mradi mkubwa wa maji  Vijijini ambao umegharimu zaidi ya shilingi bilioni 28 na utahudumia wananchi 42,000 katika wilaya SABA za mkoa wa TABORA.


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Samia Suluhu Hassan amezindua mradi mkubwa wa maji  Vijijini ambao umegharimu zaidi ya shilingi bilioni 28 na utahudumia wananchi 42,000 katika wilaya SABA za mkoa wa TABORA.

Uzinduzi wa mradi huo mkubwa na wa aina yake katika mkoa wa Tabora umetekelezwa na Serikali ya Japan kupitia Shirika lake la Maendeleo la Kimataifa (JICA) kwa ushirikiano na Serikali ya Tanzania.

Akizungumza katika halfa ya Uzinduzi wa Mradi huo katika Kijiji cha Mabama wilaya ya Uyui mkoani Tabora, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Samia Suluhu Hassan amesema kuwa nia ya Serikali ni kuona wananchi wa mkoa wa Tabora wanapata maji safi na salama karibu na maeneo yao kama hatua ya kukomesha tatizo sugu la maji kwa wananchi wa mkoa huo.

Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan amesisitiza kuwa Serikali inatambua umuhimu wa kuhakikisha wananchi kote nchini wanapata maji safi na salama kwa muda wote hivyo jitihada mbalimbali zinaendelea kuchukuliwa ili kuhakikisha tatizo sugu la maji safi la salama katika baadhi ya maeneo nchini linapata ufumbuzi wa kudumu.

Kuhusu utekelezaji duni wa baadhi ya miradi ya maji nchini, Makamu wa Rais ameonya kuwa Serikali kamwe haitawavumilia watumishi au wakandarasi ambao watatekeleza miradi ya maji ya wananchi kwa kiwango hafifu na watakaobainika watachukuliwa hatua kali za kisheria.

Amesema kuwa Serikali kwa ushirikiano na wahisani mbalimbali wamekuwa wakitoa fedha nyingi za miradi ya maendeleo hasa miradi ya maji lakini kumekuwepo na tabia ya baadhi wa watendaji wa Serikali kutumia vibaya fedha hizo na kusema kuwa muda wa watendaji hao kuiba fedha hizo umeshaisha na watakaobainika kufanya hivyo watawajibishwa ipasavyo ili kuwa fundisho kwa watu wengine.

Aidha, Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan pia amewahimiza wananchi wa mkoa wa Tabora kuutunza ipasavyo mradi huo ili uweze kuwanufaisha kwa muda mrefu wananchi wote wa mkoa huo.

Katika Hotuba yake Makamu wa Rais amewataka Viongozi wa mkoa wa Tabora kupambana ipasavyo na watu wanaoharibu mazingira hasa kwenye vyanzo vya maji kama hatua ya kuhakikisha maeneo yanahifadhiwa.

Kwa upande wake, Waziri wa Maji na Umwagiliaji Mhandisi Gerson Lwenge amesema mradi huo wa Maji Vijijini utahudumia vijiji 31 katika wilaya Saba za mkoa wa Tabora.

Waziri Lwenge ameeleza kuwa mradi huo utakuwa mkombozi mkubwa kwa wananchi wa mkoa wa Tabora kwa sababu mkoa huo ni moja ya mikoa kadhaa hapa inayokabiliwa na ukame mkubwa.

Amesema kuwa Serikali ya awamu ya Tano itaendeleo kuweka mipango na mikakati mizuri inayolenga kuhakikisha wananchi nchini wanapata maji safi na salama ili kuboresha maisha yao na kuimarisha shughuli zao za kiuchumi.

Kwa upande wake, Balozi wa Japan hapa nchini Masaharu Yoshida amesema kuwa Serikali ya Japan imetekeleza mradi huo maji ambao utanufaisha maelfu ya wananchi wa Tabora kutokana na mahusiano mazuri kati ya Tanzania na Japan.

Balozi Masaharu Yoshida amesema kuwa upatikanaji wa maji ni jambo la msingi na muhimu kwa ajili ya usalama wa binadamu na utasaidia wananchi katika shughuli za uzalishaji badala ya kutumia muda mwingi kutafuta maji.

Balozi huyo pia ameahidi Serikali ya Japan itaendelea kutoa misaada mbalimbali kwa Tanzania kufutana na matakwa ya Serikali kwa ajili ya kuboresha hali ya maisha na ustawi wa taifa na wananchi kwa ujumla.