Have you got a good story?

Share your story, discuss the issues with Dailynews Blog.

Have you got a good story?

Share your story, discuss the issues with Dailynews Blog.





Nafasi Ya Matangazo

Wednesday 9 May 2018

NDUGAI ACHARUKA BEI YA MAFUTA

Basil Msongo, Dodoma 
SPIKA wa Bunge, Job Ndugai amewataka mawaziri waseme ukweli bungeni na kwamba huo ni utamaduni wa mabunge yote.

Spika Ndugai ameyasema hayo baada ya Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage kutoa maelezo bungeni kuhusu sababu za kupanda kwa bei ya mafuta ya kula.

Ndugai amesema, kwa namna serikali inavyoshughulikia suala la bei ya mafuta inaifikisha nchi mahali pagumu sana kwa mambo madogo sana.

“Mambo madogo mno, hivi kweli nchi hii leo wale tuliosoma Chemistry pamoja na mimi, hivi kweli kupima , kupima mafuta kujua kama haya ni semi refined (safi kigodo ) ama ni crude (ghafi) hiyo nayo ni rocket science?, kitu cha dakika 15? Watu wanazunguka wanazunguka…”amesema.
 Spika amesema, kama Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) hamuamini Shirika la Viwango Tanzania (TBS), ana maabara yake, hamuamini Mkemia Mkuu mafuta hayo yakapimwe Afrika Kusini, London au Nairobi ili baada ya dakike chachge majibu yapatikane.

“Mkiligeuza Bunge hili likawa ni mahali pa kubangaiza bangaiza hivi haitakuwa sawasawa kwa hiyo saa 11 mje na maelezo ya jambo hili” amesema.

Ameshangaa kwa kusema, kupima mafuta ni suala la dakika 15 tu lakini ‘watu wanazunguka zunguka tu’.

“Tukitengeneza mazingira ya TRA mbabe mmoja anakaa anasema mimi, haiwezi kuwa hivyo, haiwezi kuwa hivyo, kama ni semi refined ipigwe kodi semi refined, kama ni crude ni crude, sasa ubishi wa nini, hakuna sababu ya ubishi, kwa hiyo tunategemea serikali saa 11 mtakuja na majibu, tunaumiza wananchi.” amesema na kuongeza kuwa hata mafuta yaliyo bandarini wananchi ndiyo watabebeshwa mzigo wa gharama.
 
Jana Waziri Mwijage aliahidi bungeni kuwa jana au leo angetoa taarifa ya Serikali kuhusu kupanda kwa bei hizo, na leo ameahidi kabla ya saa 11 jioni atampa Spika Ndugai taarifa kuhusu uchunguzi unaofanywa.

Leo wakati anatoa maelezo baada ya Mbunge wa Nzega Mjini Hussein Bashe kuomba mwongozo wa Spika, Mwijage amesema, Tanzania inazalisha asilimia 30 ya mahitaji yake ya mafuta ya kula na mengine yanaingizwa kutoka Malasyia na Indonesia.

Kwa mujibu wa kiongozi huyo, mafuta ya kula nchini yanazalishwa kwa kutumia mbegu za alizeti, ufuta, karanga na pamba.

Amewaeleza wabunge kuwa, mafuta ghafi yanayotoka nje yanatozwa kodi ya asilimia 10 na mafuta yaliyosafishwa yanatozwa 25%.

Mwijage amesema, kwenye hifadhi ya mafuta ya kula kuna tani 40,000 za mafuta ghafi lakini kuna mvutano kuhusu kiwango cha kodi kwa kuwa watalaamu wa serikali wameyapima na kutoa majibu tofauti hivyo Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) inataka kutoza kodi ya mafuta safi.

Amesema, kama TRA itatoza kodi ya mafuta ghafi Serikali itapoteza ushuru wa shilingi bilioni 22/-.

Waziri Mwijage amesema, kupima mafuta ni kazi ya muda mfupi lakini kuna utata kuhusu mafuta hayo na kwamba, kabla ya saa 11 jioni atampa jibu spika kuhusu suala hilo.

“Nakushauri Mheshimiwa Spika hili jambo unipe mimi nikawasimamie wataalamu wangu , majibu yake hapa, nitarudi kwako wewe kwamba kuna nini kabla ya saa 11 hatujarudi bungeni, hilo ndilo suala waheshimiwa linalotukumba, tunalazimika kuhakikisha kila shilingi inakusanywa, sasa wale waliotumwa kukusanya wanapoona mashaka inakuwa shida…” amesema Mwijage.
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda na Biashara, Murrad Sadick amelieleza Bunge kuwa, nyaraka zinaonesha kuwa Shirika la Viwango Tanzania (TBS) linasema mafuta hayo ni ghafi.

Amesema, nyaraka pia zinaonesha kuwa, Mkemia Mkuu wa Serikali amesema mafuta hayo ni ghafi lakini TRA wanasema si ghafi na si mafuta safi.

“Tukauliza TRA wana maabara yao?” amesema Sadick na kusema kuwa viwanda vya vya mafuta ya kula havina mafuta ghafi na bei ya bidhaa hiyo imeendelea kupanda.
Kwa Mujibu wa Bashe, bei ya mafuta ya kupikia ya Korie lita 10 imepanda kutoka sh 23,000/- hadi sh.40,000/- na bei ya mafuta hayo lita 20 imepanda kutoka sh. 50,000 hadi sh. 73,000/-.


Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Post a Comment