Have you got a good story?

Share your story, discuss the issues with Dailynews Blog.

Have you got a good story?

Share your story, discuss the issues with Dailynews Blog.





Nafasi Ya Matangazo

Saturday 25 February 2017

RAIS MUSEVENI AWASILI NCHINI NA AFANYA MAZUNGUMZO NA MWENYEJI WAKE RAIS MAGUFULI



Rais wa Jamhuri ya Uganda Mhe. Yoweri Kaguta Museveni amewasili hapa nchini leo kwa ziara rasmi ya kiserikali ya siku 2 kwa mwaliko wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli.

Katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam Mhe. Rais Museveni amepokelewa na mwenyeji wake Mhe. Dkt. Magufuli pamoja na viongozi wengine wa Tanzania Bara na Zanzibar wakiwemo Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan na Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa.

Akiwa Uwanjani hapo Mhe. Rais Museveni amepokea heshima ya kupigiwa mizinga 21 iliyokwenda sambamba na nyimbo za mataifa yote mawili na wimbo Jumuiya ya Afrika Mashariki na kisha akakagua gwaride rasmi lililoandaliwa kwa ajili yake na baadaye akashuhudia burudani ya vikundi vya ngoma na matarumbeta. 

Baada ya mapokezi hayo rasmi, Mhe. Rais Magufuli amefanya mazungumzo na mgeni wake Mhe. Rais Museveni Ikulu Jijini Dar es Salaam na baadaye viongozi wote wawili wamezungumza na wananchi kupitia vyombo vya habari.

Katika hotuba yake Mhe. Rais Magufuli amemshukuru Mhe. Rais Museveni kwa kukubali mwaliko wake wa kuitembelea Tanzania na kueleza kuwa Serikali yake ya Awamu ya Tano itaendeleza ushirikiano na uhusiano wa kidugu uliopo kati ya Tanzania na Uganda huku akitilia msisitizo wa uhusiano huo kujikita katika kuongeza biashara na kuharakisha miradi ya maendeleo inayoziunganisha nchi hizi mbili.

Mhe. Rais Magufuli amesema japo kuwa biashara kati ya Tanzania na Uganda imekua kutoka Shilingi Bilioni 178.19 mwaka 2015 hadi kufikia Shilingi Bilioni 193.59 mwaka 2016 bado nchi hizi zinapaswa kuongeza zaidi na ametoa wito kwa wafanyabiashara wa nchi zote mbili kushirikiana zaidi katika biashara na uwekezaji.

“Uwekezaji wa wafanyabiashara wa Uganda hapa nchini Tanzania una thamani ya Dola za Marekani Milioni 46.05 na umezalisha ajira 1,447”

“Watanzania wanaoishi Uganda ni wengi kuliko wanaoishi katika nchi nyingine yoyote duniani, hii ina maana tunapaswa kushirikiana zaidi na kufanya biashara zaidi” amesema Rais Magufuli.

Aidha, Mhe. Rais Magufuli amesema ili kukuza biashara na Uganda, Tanzania imeanza kutekeleza miradi mikubwa ikiwemo kujenga reli ya kati kwa kiwango cha kisasa (Standard Gauge) ambayo itakwenda pamoja na ujenzi wa bandari kavu Mkoani Mwanza ili wafanyabiashara wa Uganda wasilazimike kuja mpaka bandari ya Dar es Salaam kuchukua mizigo yao inayotoka nje ya nchi kwa meli, kukarabati meli ya MV Umoja itakayovusha mizigo mpaka bandari ya Port Bell kupitia ziwa Viktoria, kununua ndege 6 za kusafirisha kwa ajili ya Shirika la ndege la Taifa (ATCL) na kupunguza vizuizi vya barabarani hadi kufikia 3.

Kuhusu mradi wa bomba la mafuta kutoka Hoima nchini Uganda hadi Bandari ya Tanga nchini Tanzania, Mhe. Rais Magufuli amesema Tanzania ipo tayari ujenzi huo uanze baada ya kukamilisha mazungumzo ya masuala machache yaliyokuwa yamebaki na ametaka wawekezaji waanze kazi ya ujenzi badala ya kuleta visingizio.

Kwa upande wake Mhe. Rais Museveni amemshukuru Rais Magufuli kwa mapokezi mazuri aliyoyapata na amesema Uganda itaendelea kuwa ndugu na rafiki wa kweli wa Tanzania huku akisisitiza kuwa rafiki na ndugu wa kweli ni lazima wawe wamoja katika maamuzi na mipango mbalimbali ikiwemo maendeleo na biashara.

Mhe. Rais Museveni amempongeza Mhe. Rais Magufuli kwa kufuata nyayo za Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kutokana na juhudi zake za kujenga reli ya kati, kununua ndege, kufufua biashara kati ya Tanzania na Uganda na msimamo wake kuukataa mkataba wa ushirikiano wa kiuchumi kati ya nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki na Jumuiya ya Ulaya ambao umeoneka kutokuwa na manufaa ya kiuchumi kwa Afrika Mashariki ikiwemo kutishia mpango wa ujenzi wa viwanda.

“Nimefurahi kuwa Mhe. Magufuli unafuata nyayo za Mwalimu Nyerere, mimi pia ni mfuasi wa Mwalimu Nyerere, hata nilipokuja Tanzania kusoma nilikuwa namfuata Mwalimu Nyerere” amesema Mhe. Rais Museveni.

Mhe. Rais Museveni ametoa wito kwa nchi za Afrika Mashariki na Afrika nzima kuzungumza lugha moja na ziwe na msimamo wa pamoja ili kukabiliana na ukoloni ambao huko nyuma ulitawala kutokana na watawala wa Afrika kukosa umoja.

Kuhusu bomba la Mafuta, Rais Museveni amesema atafuatilia kwa ukaribu utekelezaji wa mradi huo hasa baada ya uamuzi kufanyika kuwa bomba la mafuta yaliyogundulika Hoima nchini Uganda litapitia Tanzania hadi bandari ya Tanga.

Jioni hii Mhe. Rais Museveni atahudhuria dhifa ya kitaifa iliyoandaliwa kwa heshima yake na mwenyeji wake Mhe. Rais Magufuli Ikulu Jijini Dar es Salaam.


Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Post a Comment