Have you got a good story?

Share your story, discuss the issues with Dailynews Blog.

Have you got a good story?

Share your story, discuss the issues with Dailynews Blog.





Nafasi Ya Matangazo

Tuesday 4 April 2017

SOMA ALICHOSEMA ZIITO KABWE KUFUATIA UTEUZI WA PROF. KITILA MKUMBO KUWA KATIBU MKUU WIZARA YA MAJI NA UMWAGILIAJI

BAADA ya Rais Dk John Magufuli kumteua aliyekuwa Mshauri Mkuu wa Chama cha ACT Wazalendo Prof Kitila Mkumbo kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji na Umwagiliaji, Kiongozi Mkuu wa chama hicho cha ACT Wazalendo Zitto Kabwe ameyasema haya kufuatia uteuzi huo wa Rais:- 

"Leo asubuhi Rais John Pombe Magufuli amemteua Mshauri wa Chama chetu Prof. Kitila Mkumbo kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji na Umwagiliaji.

Chama cha ACT Wazalendo kimepokea kwa mikono miwili taarifa juu ya uteuzi wa mshauri wa chama chetu Kwa sababu imeonyesha kuwa Rais ameona kuwa hata Watanzania walio kwenye Vyama vya Upinzani wana uwezo, weledi na uzalendo wa kutumikia nchi yetu. 

Kwa nafasi hii ya Ukatibu Mkuu wa Wizara, ndugu Kitila hawezi kuendelea kuwa Mshauri wa Chama nafasi ambayo inamfanya kuhudhuria vikao vyote vya Chama ikiwemo Kamati Kuu. 

Ndugu Mkumbo ameandika barua ya kujiuzulu nafasi yake ya mshauri wa Chama na kubaki kuwa mwanachama wa kawaida tu. Nimeipokea barua yake na kumkubalia Kwa maslahi mapana ya nchi yetu. 

ACT Wazalendo tunamshukuru ndugu Kitila Mkumbo kwa mchango wake katika uongozi wa Chama chetu kwa wakati wote ambao alikitumikia Chama chetu kama mshauri wa chama. 

Msimamo wa chama chetu ni utumishi wa kizalendo kwa Taifa utokanao na kila mwananchi, ndio msingi wa kaulimbiu yetu ya 'Taifa Kwanza, Leo na Kesho', hivyo basi tunamtakia kila la kheri ndugu Kitila katika utumishi wake kwa Taifa letu katika nafasi yake hii mpya. Wizara Hii ni kubwa na muhimu Sana kwa nchi yetu. 

Maji ni tatizo moja kubwa ambalo wananchi wetu wanakumbana nalo na Kama Taifa hatujaweza kulimaliza. Tunamtakia kila la kheri ndugu Mkumbo katika kuongeza nguvu kumaliza kero ya maji na kuhakikisha tunaimarisha Kilimo cha Umwagiliaji nchi nzima. 

Tunamsihi aanze na ajenda ya Mfuko wa Maji Vijijini na kuanzishwa Kwa Wakala wa Maji Vijijini utakaosimamia upatikanaji wa Maji Kwa wananchi wetu. 

Kwa hatua hii, tunaona Rais ameamua kuunganisha nchi yetu Kwa kufanya kazi na watu wote bila kuwabagua Kwa itikadi zao za vyama. Watanzania ni wamoja na kauli za kuwagawa zinaumiza zaidi Taifa kuliko kuliweka pamoja. 

Tunaamini kuwa Rais Ana nia njema katika uteuzi huu na sisi tumempa baraka zote Mwanachama wetu mwanzilishi wa Chama kwenda kwenye nafasi ya juu zaidi ya utumishi wa umma. Tunaamini hatamwangusha Rais na muhimu zaidi hatawaangusha Watanzania."

Imeandikwa na:- 
Kabwe Z. Ruyagwa Zitto
Kiongozi wa Chama - ACT Wazalendo
Aprili 4, 2017
Dodoma


Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Post a Comment