Have you got a good story?

Share your story, discuss the issues with Dailynews Blog.

Have you got a good story?

Share your story, discuss the issues with Dailynews Blog.





Nafasi Ya Matangazo

Wednesday 20 December 2017

MKURUGENZI DCB BANK AMALIZA MUDA WAKE KWA MAFANIIKIO

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Biashara ya DCB anayemaliza muda wake, Edmund Mkwawa akizungumza na wanahabari jijini Dar es Salaam jana.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Biashara ya DCB anayemaliza muda wake, Edmund Mkwawa (kulia) akiwa na Mkurugenzi Mtendaji mpya wa Benki hiyo ambaye anataraji kuanza kazi rasmi Januari mosi 2018, Godfyey Ndalahwa. Mkwawa ameiongoza benki hiyo kwa miaka 15 Tangu kuanzishwa kwake, huku akijivunia mafanikio katika utendaji wake kwa kukuza Amana za wateja kutoka shilingi Bilioni 1.76 mwaka 2002 hadi shilingi bilioni 107 Mwezi Septemba 2017. (Picha na Mroki Mroki).
************ 
MAENDELEO YA BENKI YA BIASHARA YA DCB (DCB COMMERCIAL BANK PLC) TANGU ILIPOANZISHWA MWAKA 2002

Ndugu Wanahabari
Napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutukutanisha hapa leo. Lengo la kuwaiteni ni kutoa taarifa kwa umma juu ya maendelo ya Benki ya Biashara ya DCB tangu kuanzishwa kwake ikiwemo mafanikio na malengo yake kwa kipindi kijacho kuanzia mwaka 2018.

Baadhi ya ajenda nitakazozipitia ni kutoa historia fupi ya benki na madhumuni ya uanzishwaji wake, taarifa ya utendaji kwa kipindi cha miaka 15, mahusiano na wanahisa wakuu ikiwemo manispaa ikiwemo mafanikio na changamoto iliyopata/ilizopata benki katika mahusiano hayo, msaada na uhusiano wa baadaye unaohitajika kutoka kwa wanahisa wakuu ikiwemo manispaa na mipango ya baadaye ya Benki yetu.

Awali ya yote, napenda kuwataarifu kuwa Benki ya Biashara ya DCB imekuwa mshindi wa kwanza katika mashindano ya uandaaji na uwasilishaji wa taarifa za mahesabu ya benki kwa mwaka 2016 kwa sekta za benki ndogo na za kati kwa ubora. Nafasi hii imeshikiliwa na benki yetu kwa mwaka wa pili mfululizo tangu mwaka 2015. Tuzo hii huandaliwa kila mwaka na Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Mahesabu (NBAA).

Mashindano haya yalianza tangu mwaka 2011, na katika kipindi chote hicho DCB Commercial bank imeweza kufanya vizuri ambapo kwa miaka mitatu mfululizo (mwaka 2012 hadi 2014), Benki imeshika nafasi ya tatu (3) miongoni mwa benki zote kiujumla kwa ubora wa uandaaji na uwasilishaji wa taarifa za mahesabu ya kibenki. BOFYA HAPA KUSOMA ZAIDI.


Hii ni kielelezo kwamba Benki ya DCB inafuata miongozo ya utawala bora wa fedha ikiwemo uwasilishwaji wa taarifa sahihi za amana na mikopo, kiwango cha faida kinachotumiwa katika maamuzi ya uwekezaji na ukusanywaji wa kodi; na kwa kufuata miongozo iliyowekwa na Benki kuu, Bodi ya uhasibu na viwango vya kimataifa vya uwasilishwaji wa taarifa za fedha.

Gawio la Jumla; napenda kuwakumbusha kuwa Benki ya Biashara ya DCB imetimiza miaka 15 ya utoaji huduma bora za kibenki kwa Wajasiriamali, tangu ianzishwe mnamo mwaka 2002. Ifikapo mwaka 2018 benki yetu itasheherekea miaka 16 ya utoaji huduma zake kwa wajasirimali na wanachi wenye vipato vya chini na vya kati. Katika miaka 15 ya utendaji wake, Benki ya Biashara ya DCB imekuwa ikipata faida mfululizo tangu mwaka 2004 na kutoa  gawio kwa wanahisa wake kwa miaka 10 tangu mwaka 2006 hadi 2015. Hadi kufikia mwaka 2015, jumla ya shilingi bilioni 12.4 zimetolewa kama gawio kwa wanahisa wote (Dividends) ikilinganishwa na kiwango cha shilingi milioni 681.3 zilizotolewa kama gawio kwa wanahisa kuanzia mwaka 2002 hadi mwaka 2006.

Gawio kwa Manispaa; Kama sehemu ya gawio hilo la shilingi bilioni 12.4, kiasi cha shilingi bilioni 4.4 ni gawio kwa wanahisa wake waanzilishi ambao ni Jiji la Dar es Salaam likijumuisha manispaa zake za Ilala, Kinondoni na Temeke ambao waliwekeza jumla ya shilingi Bilioni 1.3 tangu kuanzishwa kwa benki hii hadi sasa ambazo zilitoka kama asilimia 10 ya mapato ya manispaa kwa ajili ya mfuko wa wanawake na vijana. Tangu kuwekeza kiasi hicho cha shilingi bilioni 1.3, benki imekuza mtaji wa manispaa hadi kufikia shilingi 6.3 bilion kwa njia ya hisa bakizi (bonus issue) na hisa stahiki (rights issue).

Chimbuko la Benki; Ndugu wanahabari, ikumbukwe kwamba benki ya biashara ya DCB ilianzishwa kufuatia wito wa Rais wa awamu ya tatu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. Benjamin William Mkapa. Malengo ya uanzishwaji wake yakiwa ni kuwapatia mitaji wananchi wenye kipato cha chini na cha kati ambayo itasaidia kuanzisha na kuendeleza biashara zao.
Hivyo basi, benki ya biashara ya DCB inaendelea kutimiza wajibu wake kwa ufasaha na weledi kwa kuanzisha huduma mbalimbali za kibenki zinazokidhi mahitaji ya kifedha na hivyo kutimiza ndoto za wananchi.

Benki imekuwa ikiwakopesha Wanawake na Vijana na vikundi mbalimbali kupitia mfuko wa Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni, Temeke na Ilala ambapo hadi mwaka 2017 Shilingi bilioni 123.8 zimeshatolewa kwa wanufaika 476,146. Kati ya hizo, shilingi bilioni 12.7 zinatokana na mfuko wa Manispaa za Dar es Salaam. Benki inatarajia kuendelea kukuza mikopo kupitia mifuko hii na inaendelea kushirikiana na kuhamasisha manispaa ziendelee kutunisha mfuko huu kwa manufaa ya wananchi.

Mtandao wa Benki; Benki imepanua wigo wake wa biashara kutoka benki inayotoa huduma zake Dar es salaam pekee, na kuwa benki ya kibiashara inayotoa huduma zake nchi nzima kwa kuanzisha huduma zenye kurahisisha upatikanaji wa huduma za DCB kupitia wakala (DCB Jirani) na huduma kupitia simu ya mkononi (DCB Pesa).

Huduma ya DCB Jirani inaendelea vizuri kwa sasa Benki ina jumla ya mawakala 542 wanaotoa huduma za DCB nchi nzima. Huduma hizi zitasaidia kuwafikia wateja wengi Zaidi na kwa gharama nafuu na itaweza kuwafikia jamii ya watanzania wa kipato cha chini na cha kati ambao ni Zaidi ya asilimia 70. Benki hii pia imejikita katika kusogeza huduma kwa wateja kupitia matawi, ambapo matawi yameongezeka kutoka matawi 2 mwaka 2005 hadi matawi 8 mwaka 2017. Mwezi April 2017 benki imefungua tawi la 8 makao makuu ya nchi, Dodoma.

Thamani ya Hisa; Benki ya DCB ndio benki ya kwanza kuorodheshwa katika soko la hisa la Dar es Salaam mnamo mwaka 2008. Pamoja na mabadiliko ya hali ya soko la hisa la Dar es Salaam kwa kipindi cha utendaji wa benki, hadi kufikia robo ya tatu ya mwaka huu (2017) thamani ya hisa kwenye soko imefikia shilingi 380 ikiwa imeongezeka kutoka shilingi 275 (mwaka 2008). Benki iliongoza kwa kufanya vizuri katika soko la hisa la Dar es Salaam mwaka 2011 kwa kuwa Benki ya Kwanza Afika Mashariki na ya tano Afrika.
Mahusiano na Wanahisa; Benki imeendelea kuwa na mahusiano mazuri na wanahisa ukiacha changamoto chache zilizojitokeza kuhusiana na pesa za mgao kutoka manispaa na nafasi ya manispaa katika kuwekeza amana zake katika benki. Hata hivyo, Benki na manispaa zimefanya vikao mbalimbali vilivyolenga kuondoa sintofahamu iliyokuwepo na pia kuwaelimisha wadau wapya wa manispaa mafanikio na malengo ya muda mrefu ya Benki ambayo wengi hawakuwa wakiyafahamu. Tuna Imani thabiti kuwa mahusiano yataboreka na kusaidia Benki kukua Zaidi kiutendaji.
Utendaji; Tangu kuanzishwa kwake, benki ya biashara ya DCB imepata mafanikio ya katika utendaji wake kwa kukuza Amana za wateja kutoka shilingi Bilioni 1.76 mwaka 2002 hadi shilingi bilioni 107 Mwezi Septemba 2017. Mikopo ya benki pia imeongezeka kutoka shilingi Bilioni 1.02 mwaka 2002 hadi kufikia shilingi Bilioni 89.2, mnamo Mwezi Septemba 2017.

Msaada kwa Jamii; Jumla ya shilingi milioni 180.3 zimetumika kusaidia shughuli mbalimbali kwa manufaa ya Jamii kama vile msaada wa Vitanda, vyandarua, mashine za kupumulia watoto, vitanda kwa ajili ya akina mama kujifungua katika Hospitali za manispaa za Dar es salaa, madawati, vifaa vya maabara mashuleni.

Ili kusaidia ukuaji wa uchumi wa viwanda, Benki imelipa kodi, tozo na makato mbalimbali serikalini ambazo zinafikia shilingi Bilioni 23.4 kwa kipindi cha mwaka 2002 hadi 2016.

Changamoto; Mnamo mwaka 2016, benki haikufanikiwa kutoa gawio kwa wanahisa wake ikiwa ni mrejeo wa changamoto mbalimbali ambazo benki ilikutana nazo katika utendaji wake. Chache kati ya hizo ni benki kupoteza wateja wakubwa wa serikali ambao walifunga akaunti na kuzihamishia benki kuu, idadi kubwa ya mikopo chechefu iliyotokana na watumishi hewa wa serikali ambao sehemu kubwa walikuwa na mikopo katika benki yetu na pia kuongezeka kwa gharama zisizotokana na riba zinazohusiana na ushuru katika huduma za kila siku. Sababu zote hizi zilisababisha matokeo yasiyoridhisha na kupelekea benki kupata hasara katika mwaka 2016.


Mipango ya baadaye; Benki itaendelea kutumia fursa mbalimbali za kiuchumi zinazojitokeza hasa katika mikopo ya wajasiriamali wadogo na wa kati ili kuwainua kiuchumi kupitia mitaji yenye masharti nafuu na wezeshaji Kwa kuongezea, benki itaendelea kushirikiana na mifuko mbalimbali maalumu ikiwemo manispaa zote tano za Jiji katika kusaidia maendeleo ya vikundi vya wajasiriamali wadogo ikiwemo wanawake na vijana.
Kwa kufanya hayo, benki itakuwa imesaidia ukuaji wa uchumi wa wanyonge na wasiojiweza ilhali ikitekeleza hatua muhimu ambazo ni muafaka kwa mazingira yaliyopo. Malengo na maslahi ya wanahisa na wadau wote yatalindwa huku benki ikiendelea kukuza amana kwa kuwa na amana za kudumu na ambazo ni za gharama nafuu. Wakati huohuo benki itajikita katika kuhakikisha inakusanya mikopo chechefu huku ikikuza mikopo yenye ubora ambayo itailetea benki mapato.

Ndugu Wanahabari;
MATARAJIO YA MWAKA 2018
Benki imejipanga kuendeleza malengo yake na kuhakikisha inakuwa chaguo la kwanza la wateja katika utoaji huduma za kifedha. Katika kutimiza malengo haya, benki itatumia teknolojia ya kisasa katika utoaji wa huduma zake kupitia huduma ya DCB Pesa (kupitia simu ya mkononi) na DCB Jirani (Huduma kupitia wakala) kwa lengo la kuwafikia wateja wengi walengwa ambao ni wajasiriamali wadogo na wa kati waliosambaa kote nchini hadi vijijini.

Mojawapo ya malengo ya benki kwa mwaka unaokuja wa 2018 ni kuhakikisha inaongeza wigo na viwango vya utoaji huduma na kuwafikia wateja wengi zaidi wanaohitaji huduma za kibenki ikiwemo wamiliki wa Vikoba na Wafanyabiashara wa kati ambao wamehitimu hatua za mikopo ya awali katika benki hii. Hii ni kuhakikisha benki inakua pamoja na wateja wake na haitowaacha kuwahudumia katika mahitaji yao hata wakiongeza wigo wa biashara zao.

Kwa kuongezea, Benki itaendelea kukuza amana na mikopo kwa wateja ili kujiwekea mazingira mazuri ya kiutendaji na kuiwezesha kuchangia maendelo ya nchi kupitia utoaji wa gawio kwa wanahisa, ulipaji wa kodi za serikali na utoaji wa ajira kwa wananchi. Ili kufanikisha hayo, benki itawekeza katika rasilimali watu kusaidia uboreshwaji wa huduma za mikopo ya vikundi vya wanawake na vijana na mikopo ya vikoba.

Benki itaendelea kuwekeza katika teknolojia ili kuhakikisha inatoa huduma za kisasa kupitia mawakala na simu za mikononi ili kuwafikia walengwa wa mikoani na vijijini. Kwa kuhitimisha, benki itajitahidi kudhibiti mikopo chechefu na kukusanya madeni ya wateja yaliyopitiliza muda ili kusaidia kuimarisha mtaji na kutoa huduma kwa wateja wengine.


Hitimisho
Uongozi wa benki unapenda kuwataarifu kuwa Mkurugenzi wa awali aliyeianzisha na kuifikisha hapa benki ya biashara ya DCB Bw. Edmund Mkwawa anatarajia kustaafu kuanzia tarehe 31 Desemba 2017. Kuanzia hapo, benki itakuwa chini ya usimamizi wa mkurugenzi anayeshika hatamu Bw. Godfrey Ndalahwa.
 
Benki ya Biashara ya DCB inapenda kuwatakia wateja wake, wadau, wanahisa na wananchi kwa ujumla sikukuu njema ya Christmas na heri ya mwaka mpya 2018.

EDMUND P. MKWAWA
MKURUGENZI MTENDAJI
DCB COMMERCIAL BANK PLC

DESEMBA 2017.


Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Post a Comment