VILIO, Majonzi na Simanzi vimetawala
katika viunga vya Bunge jijini Dodoma hii leo kufuatia kifo cha Mbunge wa Jimbo
la Buyungu, Mwalimu Kasuku Bilago. Anaandika Mroki Mroki – Daily News Digital,
Dodoma
Mwalimu Bilago alifikwa na umauti wakati
akipata matibabu katika Hospitali ya Taifa Muhimbili Jumamosi Mei 26, mwaka huu
jijini Dar es Salaam.
Muda mfupi baada ya Naibu Spika wa Bunge Dk. Tulia Ackson kufungua kikao cha Bunge kwa kusoma dua, alitoa Bungeni hapo Taarifa ya Spika kuhusiana na msiba huo mzito uliolifika Bunge, naabade kutangaza kuahirisha Bunge hadi Mei 29 saa tatu asubuhi, ili kupisha Maombolezo huku mipango ya kuuleta mwili katika viwanja vya Bunge kwa heshima za mwisho ikifanyika.
Daily News Digital ilishuhudia wabunge
wakitoka Bungeni huku wakiwa na nyuso za huzuni na wengi wao wakibubujikwa na
machozi na vilio vya kwikwi.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejiment
ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, George Mkuchika amemtaja marehemu kuwa ni
miongoni mwa wabunge Bora ambao walikuwa wakijenga hoja na kutoa michango yenye maslahi mapana kwa
Jimbo lake na nchi kwa ujumla.
Nae Mbunge wa Mikumi, Joseph Haule
alizungumzia msiba huo na kusema ni pengo kubwa Mwalimu Bilago ameliacha si kwa
Kambi ya Upinzani bali kwa Bunge zima kutokana na mchango wake aliokuwa
akiutoa.
“Mwalimu Bilago alikuwa Mwalimu kweli
kweli, hakuna siku ambayo alisimama kuchangia asipate sapoti ya Bunge zima nah
ii ni kutokana na ucheshi wake lakini pia hoja zake za msingi alizokuwa
akizitoa Bungeni,”alisema Haule.
Mwili wa Marehemu Bilago unataraji kuletwa
Bungeni Mei 29 kwa heshima za mwisho na baade kusafirishwa hadi Kijiji cha
Kasuga Wilaya ya Kakonko Mkoani Kigoma ambako utahifadhiwa Mei 30 mwaka huu.
Wabunge mbalimbali wakifarijiana kufuatia Msiba huo mzito wa Mwezao.
Mawaziri wakiweka saini katika kitabu cha maombolezo cha Mbunge Kasuku Bilago wa Jimbo la Buyungu, Wilayani Kakonko mkoa wa Kigoma.
Wabunge wakisaini kitabu cha maombolezo
Kuna Maoni 0 mpaka sasa.
Post a Comment