Have you got a good story?

Share your story, discuss the issues with Dailynews Blog.

Have you got a good story?

Share your story, discuss the issues with Dailynews Blog.





Nafasi Ya Matangazo

Monday 23 April 2018

Rais Magufuli afungua jengo la PSPF, Ofisi ya makao makuu NMB Dodoma


 Jengo la ghorofa 12 la PSPF DODOMA PLAZA
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli leo tarehe 23 Aprili, 2018 amefungua jengo la mfuko wa hifadhi ya jamii wa PSPF, ofisi ya makao makuu ya benki ya NMB Mjini Dodoma na matawi mawili ya benki hiyo. 

Jengo la PSPF lenye ghorofa 11 lina ukubwa wa mita za mraba 15,741.60, limejengwa kwa gharama ya Shilingi Bilioni 30.56 na ndani ya jengo hilo ndimo benki ya NMB imefungua ofisi zake za makao makuu, tawi la benki kwa wateja maalum, na tawi la benki kwa wateja binafsi lililopewa jina la Kambarage kwa lengo la kumuenzi Baba wa Taifa Hayati Mwl. Julius Kambarage Nyerere.

Mkurugenzi Mkuu wa PSPF Bw. Adam Mayingu amesema jengo hilo ambalo tayari limeshapata wapangaji kwa asilimia 98 wengi wao wakiwa ofisi za umma, linatarajiwa kuzalisha Shilingi Bilioni 4.7 kila mwaka na litarejesha fedha za uwekezaji ndani ya miaka 8 na kwamba katika juhudi hizo hizo za kuunga mkono Serikali kuhamia Dodoma PSPF inatekeleza mradi mwingine wa ujenzi wa nyumba 500 kwa ushirikiano na mfuko wa hifadhi ya jamii wa Watumishi Housing.

Mkurugenzi Mtendaji wa benki ya NMB Bi. Ineke Bussemaker amesema benki hiyo yenye matawi 218 ndio benki kubwa inayoendeshwa kwa faida hapa nchini na ikiwa na kiwango kidogo cha mikopo chechefu, imekuwa ikichangia katika bajeti ya nchini kupitia kodi na gawio ambapo katika miaka mitatu iliyopita imechangia Shilingi Bilioni 16.525 kila mwaka na katika sherehe hizo amechangia Shilingi Milioni 50 kwa maendeleo ya Dodoma.

Akizungumza kwa niaba ya Mke wa Baba wa Taifa Mhe. Mama Maria Nyerere, Mtoto wa Baba wa Taifa Bw. Makongoro Nyerere ameishukuru benki ya NMB kwa kutambua mchango wa Baba wa Taifa na kuamua tawi hilo liitwe jina lake la “Kambarage” na pia ametoa wito kwa vijana kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Mhe. Rais Magufuli.

“Mhe. Rais wewe chapa kazi, hawa wanaokushambulia hata wakati wa Baba wa Taifa walikuwepo na wengine walikimbilia nchi nyingine, wewe chapa kazi” amesisitiza Bw. Makongoro Nyerere.

Akihutubia kabla ya kufungua rasmi miradi hiyo, Mhe. Rais Magufuli ameipongeza PSPF kwa kuwekeza katika jengo ambalo tayari limeshapata wapangaji na pia ameipongeza mifuko ya hifadhi ya jamii kwa kuitikia wito wa kuwekeza katika viwanda 16 ambavyo vitazalisha ajira na kuchangia katika uchumi wa nchi.

Mhe. Rais Magufuli pia ameipongeza benki ya NMB kwa kazi nzuri inayofanya na kwa kuwafikishia huduma Watanzania wengi, lakini ametaka katika mwaka huu wa 2017/18 benki hiyo inayomilikiwa na Serikali kwa asilimia 32 iongeze gawio.

“Mwaka 2012/13 Benki ya NMB ilitoa gawio kwa Serikali la Shilingi Bilioni 10.805, mwaka 2013/14 ikatoa Shilingi Bilioni 14.301, mwaka 2014/15 ikatoa Shilingi Biliongi 16.525, mwaka 2015/16 ikatoa gawio hilohilo la Shilingi Bilioni 16.525 na mwaka 2016/17 ikatoa tena gawio hilohilo la Shilingi Bilioni 16.525, yaani miaka mitatu mfurulizo mnatoa gawio lilelile wakati mnatuambia faida ya benki imekua, nataka mnaoiwakilisha Serikali kwenye NMB mkaliangalie hili na gawio la mwaka 2017/18 liongezeke” amesema Mhe. Rais Magufuli.

Aidha, Mhe. Rais Magufuli amejibu ombi lililotolewa na Mbunge wa Dodoma Mjini Mhe. Anthony Mavunde la kupunguzwa kwa tozo ya kodi katika mchuzi wa zabibu, na amewataka wadau wanaohusika wakiwemo wabunge kufanyia kazi ombi hilo kwa zao la zabibu na mazao mengine ya kilimo na mifugo hapa nchini ili tozo za kodi zisisababishe bidhaa za wazalishaji wa Tanzania kushindwa kushindana na bidhaa zinazoingizwa nchini kutoka nje ya nchi.

Mhe. Rais Magufuli pia amemshukuru Mtoto wa Baba wa Taifa Bw. Makongoro Nyerere kwa ujumbe wake kwa Watanzania hasa vijana na amemhakikishia kuwa Serikali anayoiongoza ipo imara na itaendelea kuwa imara kusimamia misingi ya kulijenga Taifa.


Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Post a Comment