Have you got a good story?

Share your story, discuss the issues with Dailynews Blog.

Have you got a good story?

Share your story, discuss the issues with Dailynews Blog.





Nafasi Ya Matangazo

Monday 26 June 2017

WAZIRI MKUU APIGA MARUFUKU USAFIRISHAJI WA CHAKULA NJE YA NCHI

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amepiga marufuku usafirishaji wa chakula kwenda nje ya nchi kuanzia leo. 

“Kuanzia leo, ni marufuku kwa mtu yoyote kusafirisha mazao ya chakula kwenda nje ya nchi bila ya vibali. Serikali inahamasisha uwekezaji kwenye ujenzi wa viwanda nchini. Kama tutatoa vibali, ni lazima mtu alazimike kusaga nafaka ili kutoa ajira nchini,” amesema. 

Waziri Mkuu ametoa agizo hilo leo (Jumatatu, Juni 26, 2017) wakati akitoa nasaha kwenye Baraza la Eid lililofanyika kitaifa kwenye msikiti wa Masjid Riadha, mjini Moshi, mkoani Kilimanjaro mara baada ya kuswali sala ya Eid. 

“Jana nimeona kwenye televisheni taarifa kuhusu malori 10 yaliyokamatwa Tarakea yakiwa na mahindi tayari kuvushwa mpaka. Mheshimiwa RC akasema chakula hicho ni lazima yarudishwe kwa ajili ya usagaji.”

“Mimi nasema kuanzia leo, yeyote atakayekamatwa akitorosha chakula kwenda nje ya nchi, chakula hicho kitataifishwa na kupelekwa ghala la Taifa na gari lake tutalitaifisha na litaishia Jeshi la Polisi. Tunafanya hayo kwa lengo la kuwalinda Watanzania tusikumbwe na baa la njaa.” 

Akitoa tahadhari kuhusu uuzwaji wa chakula nje ya nchi, Waziri Mkuu amesema kumekuwa na wimbi kubwa la usafirishaji wa chakula kwenda nje ya nchi bila kibali. “Hilo ni kosa kubwa kwa sababu litasababisha nchi yetu kupata baa la njaa huko mbele,” amesema.

Amesema mipaka ya Tarakea, Holili, Mwanga, Horohoro, Siha, Namanga na Sirari imekuwa inapitisha kiasi kikubwa cha mazao ya chakula kwenda nje ya nchi jambo ambalo ni hatari sana. “Hii ni kwa sababu chakula cha ndani hakitoshelezi mahitaji. Kwa sababu nchi zote za jirani hazina chakula cha kutosha. Tusipokuwa makini, tutabaki tunalia njaa."

Waziri Mkuu ametumia fursa hiyo kuwasihi wafanyabiashara wa ndani, wachukue mahindi kutoka maeneo yenye mavuno mengi na kuyapeleka kwenye sehemu zenye mavuno kidogo. “Watanzania tushirikiane, kama ni biashara tutoe huku kwenye mavuno mengi na tuyapeleke Shinyanga na Geita ambako wanayahitaji au tukanunue Sumbawanga na kuyapeleka kwenye mikoa mingine yenye upungufu,” alisisitiza. 

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amewataka viongozi wa dini waisadie Serikali katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya kwa kupitia kwenye nyumba za ibada. “Naomba tuendelee kushirikiana kupambana na janga hili la dawa za kulevya kwa ustawi wa nchi yetu. Naamini viongozi wa dini mnayo nafasi kubwa katika mapambano haya, kwa kuwafunda vijana wetu kuishi katika maadili ya kidini na kutojiingiza kwenye janga hilo.”

Alisema Serikali kwa upande wake itaendeleza mapambano hayo bila ajizi wala mzaha. “Tunaomba wananchi wote watuunge mkono kwa kutoa taarifa sahihi za wanaojihusisha na uzalishaji, utengenezaji, usambazaji na utumiaji wa dawa za kulevya pindi tu wanapowabaini.”

Wakati huo huo, akitoa tafsiri ya Qur’aan tukufu kwenye Baraza la Eid, Sheikh wa Mkoa wa Arusha, Sheikh Shaaban Juma alisema kila nguzo katika Uislamu inapaswa kufuatwa na kwamba mtu akiharibu nguzo moja tu anakuwa ameharibu nguzo zote tano.

Alisema siku ya kiyama, watatokea watu wenye thawabu kama milima ya Usambara ama Upareni na akawataka Waislamu wote nchini wadumu katika kutenda mema ili wapate thawabu.

Mapema, akitoa khutba katika swala ya Eid el Fitr iliyoswaliwa kwenye msikiti huohuo wa Masjid Riadha, Sheikh Mlewa Shaban alisema sikukuu ya Eid ni siku ya kujiepusha na madhambi kama ulevi, kamari na lugha chafu, bali aliwataka waumini wote waitumie siku hiyo kuwapa furaha maskini, yatima na wajane.

“Mtu asiseme mwezi wa Ramadhan umepita, sasa narudia mambo yangu ya zamani. Adhabu za Mwenyezi Mungu hazina mipaka na wale waliotulizana watapata thawabu yao, kumbukeni neema na Mwenyezi Mungu na mcheni Mwenyezi Mungu.”

“Kitu tunachopaswa kufanya kila wakati ni kumcha Mwenyezi Mungu. Lazima tupendane, tuondoe tofauti zetu na tuujenge Uislam. Hatuwezi kuujenga uislam kama hatupendani. Lazima tuilinde ibada yetu kwa sababu hatuna garantii, ni lini tutaondoka,” alisema.

Sherehe hizo zilihudhuriwa na Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania, Sheikh Abubakar Zubeir bin Ally; Wajumbe wa Baraza la Ulamaa, Waziri wa Maliasili na Utalii, Prof. Jumanne Maghembe; Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Mama Anna Mghwira; IGP Mstaafu, Bw. Said Mwema; Mbunge wa Moshi Mjini, Bw. Jaffary Michael; Wakuu wa Wilaya za Mkoa huo na viongozi mbalimbali wa dini na Serikali.


Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Post a Comment