Have you got a good story?

Share your story, discuss the issues with Dailynews Blog.

Have you got a good story?

Share your story, discuss the issues with Dailynews Blog.





Nafasi Ya Matangazo

Sunday 5 March 2017

RAIS MAGUFULI ATOA MAAGIZO MAZITO WIZARA YA NISHATI NA TANESCO



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Dkt. John Pombe Magufuli ametoa siku 7 kwa Wizara ya Nishati na Madini kumega eneo lenye makaa ya mawe katika eneo la Ngaka lililopo Wilaya ya Mbinga Mkoani Ruvuma na kuipatia kampuni ya Dangote ili iweze kuzalisha yenyewe makaa ya mawe kwa ajili ya kiwanda chake cha saruji kilichopo Mkoani Mtwara.

Mhe. Rais Magufuli ametoa agizo hilo leo tarehe 05 Machi, 2017 wakati wa uzinduzi wa magari 580 ya kusafirishia saruji ya Kampuni ya Dangote uliofanyika kiwandani hapo na kuhudhuriwa na Waziri wa Nishati na Madini Prof. Sospeter Mwijarubi Muhongo, Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Isdor Mpango na Mmiliki wa kiwanda cha Dangote Alhaji Aliko Dangote.

Pamoja kuagiza kampuni ya Dangote ipatiwe eneo la kuchimba makaa ya mawe, Mhe. Dkt. Magufuli ameitaka Wizara ya Nishati na Madini kuhakikisha inafikisha gesi katika kiwanda hicho haraka iwezekanavyo lengo likiwa kuondoa vikwazo vya uhaba wa makaa ya mawe na ukosefu wa gesi ambavyo vimekuwa vikisababisha uzalishaji wa saruji kusimama mara kwa mara.

Mhe. Rais Magufuli pia ameitaka kampuni ya saruji ya Dangote kuwasiliana moja kwa moja na Serikali pale inahitaji huduma yoyote badala ya kuwatumia watu wa kati ambao wamekuwa wakisababisha kuongezeka kwa gharama za uendeshaji na bidhaa na hivyo kuathiri uzalishaji wa saruji wa kiwanda hicho.

 Kabla ya kuzindua rasmi magari hayo Mhe. Rais Magufuli amepokea kero za madereva ambao walifanya usaili wa kuomba kazi ya kuendesha magari hayo tangu miezi miwili iliyopita, ambapo wamemueleza kuwa menejimenti ya kiwanda hicho haijawaita kazini mpaka leo licha ya kuwepo kwa malori mapya wanayopaswa kuendesha, huku Menejimenti ikiendelea kutumia malori ya watu binafsi kupitia kampuni za kati ambazo ndizo zimekuwa zikitumika kutoa huduma nyingi kwa kiwanda.

Kufuatia malalamiko hayo Mhe. Dkt. Magufuli amemshauri mmiliki wa kiwanda hicho Alhaji Aliko Dangote kuiangalia vizuri Menejimenti yake na kuitaka iachane na wafanyabiashara wa kati ikiwemo kampuni moja iliyotaka kupewa zabuni ya kupokea gesi kutoka Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) kisha kuzalisha umeme na kuiuzia Dangote.

"Ndugu Alhaji Aliko Dangote, iangalie vizuri Menejimenti yako, inawatumia watu wa kati na ndio hao wanaosababisha matatizo, na mimi nimeshaiagiza wizara hakuna kuuza gesi kwa watu wa kati, tunataka tukuletee gesi wewe mwenyewe na uzalishe umeme wewe mwenyewe" amesisitiza Rais Magufuli.

Kwa upande wake Alhaji Aliko Dangote ameelezea kufurahishwa kwake na uwekezaji wa kiwanda hicho uliogharimu Dola za Marekani Milioni 650 na kwamba kiwanda hicho kitakachozalisha tani Milioni 2 za saruji mwaka huu kinatarajia kufikia uzalishaji wa tani Milioni 3 mwaka ujao, kuzalisha ajira 20,000 huku kikiwa kimesaidia kupunguza bei ya saruji nchini kutoka Shilingi 15,000/- kwa mfuko mmoja kilo 50 hadi kufikia Shilingi 10,000/-.

Alhaji Aliko Dangote ameongeza kuwa tangu kampuni yake ianze kuuza saruji bei ya bidhaa hiyo sokoni imeshuka kutoka Shilingi 15,000/- kwa mfuko mmoja wa kilo 50 hadi kufikia Shilingi 10,000/- na kwamba imeamua kununua magari ya kusafirisha saruji ili iweze kusambaza saruji hiyo nchi nzima kwa gharama nafuu ambayo watanzania wengi wataimudu.

Nae Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Mpango amesema licha ya kuzalisha ajira, tangu kampuni hiyo ianze shughuli zake imeshalipa kodi kiasi cha Shilingi Bilioni 46.139 na kodi inatarajiwa kuongezeka kadiri uzalishaji unavyopanda.

Wakati huo huo, Mhe. Rais Magufuli amezindua kituo cha kupooza umeme cha Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kilichopo mjini Mtwara ambacho kinajengwa kwa fedha na wataalamu wa TANESCO kwa gharama ya Shilingi Bilioni 16, mradi ambao utahusisha ujenzi wa njia ya umeme ya kilovoti 132 kutoka Mtwara hadi Lindi na hivyo kumaliza tatizo la kukatika kwa umeme katika Mji wa Lindi.

Mhe. Dkt. Magufuli amempongeza Waziri wa Nishati na Madini Prof. Sospeter Mwijarubi Muhongo, Menejimenti na wafanyakazi wa TANESCO kwa kazi nzuri wanayofanya iliyowezesha usambazaji wa umeme kuongezeka hadi kufikia asilimia 46 ya nchi nzima, lakini ametoa maagizo kwa TANESCO kuwakatia umeme wote wenye madeni bila kujali kama ni taasisi ya umma ama binafsi.

Mapema leo asubuhi Mhe. Rais Magufuli amesali ibada ya Diminika ya kwanza ya Kwaresma katika Kanisa la Watakatifu wote, Jimbo Katoliki la Mtwara ambako amechangia Shilingi Milioni 1 na mifuko 200 ya saruji kwa ajili ya ujenzi wa uzio wa Kanisa na ukarabati wa Kanisa na amewataka wananchi wa Mtwara kushikamana kuiombea nchi na kufanya kazi kwa ajili ya maendeleo ya mkoa na Taifa zima.


Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Post a Comment