Have you got a good story?

Share your story, discuss the issues with Dailynews Blog.

Have you got a good story?

Share your story, discuss the issues with Dailynews Blog.





Nafasi Ya Matangazo

Friday 18 May 2018

WAZIRI MPINA ABAINI UPOTEVU WA BILIONI 263 UTOROSHAJI MIFUGO NJE YA NCHI

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Luhaga joelson kulia akiwa na Mkuu wa Wilaya ya Longido Daniel Chongolo wakiwa kwenye  bango la uzinduzi wa Operesheni Zagamba 2018. Operesheni hiyo  ni maalum kwa ajili ya kudhibiti utoroshaji wa mifugo na mazao yake nchini, ambapo kitaifa ilizinduliwa Namanga kwenye Wilaya ya Longido. Picha na John Mapepele
Waziri wa Mifugo na Uvuvi Luhaga joelson kulia akitoa maelezo ya maana ya Operesheni Nzagamba2018 kwenye  bango la uzinduzi wa Operesheni Zagamba 2018. Operesheni hiyo  ni maalum kwa ajili ya kudhibiti utoroshaji wa mifugo na mazao yake nchini, ambapo kitaifa ilizinduliwa Namanga kwenye Wilaya ya Longido. Picha na John Mapepele

Na John Mapepele, Arusha
WAZIRI wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina amesema Serikali kila mwaka inapoteza jumla ya sh bilioni 263 kila mwaka kufuatia kushamiri kwa utoroshaji wa mifugo nje ya nchi na uingizaji wa mazao ya mifugo usiozingatia sheria na taratibu za nchi hali inayochangia ushindani usio wa haki kwa wazalishaji wa ndani ya nchi.

Akizungumza jana kwenye mnada wa mifugo wa Namanga wilayani Longido mkoani Arusha wakati wa uzinduzi wa operesheni maalum ya kitaifa ya kudhibiti upotevu wa mapato na usimamizi wa biashara ya mifugo na mazao yake iliyopewa jina la ‘Operesheni Nzagamba 2018’ Waziri Mpina alisema operesheni hiyo itamfikia kila mtu anayejishughulisha na tasnia nzima ya mifugo.

Alisema operesheni hiyo itafika kwenye minada ya mifugo, bandarini, viwanja vya ndege, mipakani, kwenye masoko na maduka,supermarket, na machinjioni ili kujiridhisha na uhalali wa biashara hiyo.

Pia Waziri Mpina alisema operesheni hiyo imefanikiwa kubaini kuwepo kwa ubabaishaji mkubwa unaofanywa na baadhi ya wafanyabiashara kufanya udanganyifu katika biashara ya dawa za mifugo,upotevu mkubwa wa mapato na uingizaji holela wa mazao ya mifugo kutoka nje ya nchi ikiwemo nyama na maziwa kupitia njia za panya.

Akitolea mfano eneo la Namanga zaidi ya mbuzi 22,000 zilikamatwa zikitoroshwa kwenda nchini Kenya huku makusanyo yakiongezeka na kufikia sh milioni 200 kwa muda wa mwezi mmoja tangu kuanza operesheni hiyo ambapo kwa upande wa Mwanza makusanyo yameongezeka kutoka sh milioni 17 kwa mwezi na kufikia Sh. Milioni 532.

Waziri Mpina alisema tathimini ya awali iliyofanywa na wizara yake imebaini kuwa wastani wa ng’ombe milioni 1.6 hutoroshwa kila mwaka kwenda kuuzwa nchi za jirani ambapo Serikali hupoteza sh bilioni 56.4 kwa mwaka huku upande wa ngozi Serikali ikipoteza sh. Bilioni 87.6 kwa mwaka ambapo kwa upande wa nyama na maziwa Serikali hupoteza zaidi ya sh bilioni 120 kila mwaka

Aidha alionya kuwa mifugo itakayokamatwa ikitoroshwa kwenda nchi jirani kinyume cha sheria Serikali itafanya maamuzi magumu ya kutoza faini kubwa ili kuhakikisha watu wote wanafuata sheria ili mifugo hiyo iweze kunufaisha watanzania wote kupitia mfumo wa ushuru na kodi.

Kuhusu tozo ya mifugo inayokwenda nchi za nje, Waziri Mpina alisema msimamo wa Serikali unabaki pale pale ambapo kila ng’ombe atatakiwa kulipiwa sh 20,000 na Mbuzi sh. 5,000 huku akiruhusu vibali vya biashara za mifugo vinavyotolewa na halmashauri viendelee kutumika hadi pale Wizara ya Mifugo na Uvuvi itakapoamua vinginevyo.

Pia Waziri Mpina alipongeza uamuzi wa kujengwa kwa mnada wa kisasa wa mifugo katika eneo hilo la uliofadhiliwa na Mradi wa MIVARF na kugharimu sh. Milioni 782 na kusisitiza kuwa mnada huo utakuwa mkombozi mkubwa kwa wafugaji kupata soko la uhakika la mifugo yao.

Kaimu Katibu Mkuu Mifugo, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dk Lovince Assimwe alisema operesheni hiyo imewezesha kubaini mianya ya upotevu ya mapato yatokanayo na sekta ya mifugo na kusisitiza kuwa itakuwa endelevu hadi pale wadau wa sekta hiyo watakapofuata sheria za nchi.

Dk Assimwe Serikali ya awamu ya tano chini ya Dk. John Pombe Magufuli imedhamiria kwa dhati kusimamia sekta ya mifugo ili iweze kutoa mchango unaostahili kwa maendeleo ya Taifa.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Longido, Daniel Chongolo alimshukuru Waziri Mpina kwa juhudi kubwa anazofanya za kudhibiti utoroshaji wa mifugo na kumhakikishia kuwa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya wilaya hiyo itaendelea kushirikiana na wizara kuhakikisha mifugo haiendi nje ya nchi kwa njia za panya.

Alisema maagizo yote yaliyotolewa na Waziri Mpina atatumia uwezo wake wote kuhakikisha yanasimamiwa kikamilifu ili kuweza kupata matokeo mazuri yanatoyarajiwa.


Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Post a Comment