Have you got a good story?

Share your story, discuss the issues with Dailynews Blog.

Have you got a good story?

Share your story, discuss the issues with Dailynews Blog.





Nafasi Ya Matangazo

Friday 19 May 2017

MAKAMU WA RAIS AAGIZA UHAKIKI KWA WALIOPEWA HATI MAENEO OEVU

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Samia Suluhu Hassan ameagiza kufanyika kwa uhakiki wa hati za hakimiliki zote zilizotolewa kwenye ardhi oevu na kuzibatilisha haraka iwezekanavyo ili kuokoa ikolojia ya Bonde la Mto Ruaha Mkuu.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Samia Suluhu Hassan ametoa agizo hilo mjini Dodoma wakati wa kupokea Taarifa ya Kikosi Kazi cha Kitaifa cha Kuokoa Mifumo wa Ikolojia ya Bonde la Mto Ruaha Mkuu kilichoundwa na Ofisi yake ili kukoa uharibifu mkubwa wa mazingira unaoendelea katika Bonde la Mto Ruaha Mkuu.

Makamu wa Rais Mhe Samia Suluhu Hassan pia ameagiza watendaji wa ofisi yake ushirikiane na Tamisemi wahakikishe wanawaondoa watu wote waliovamia maeneo ya hifadhi ya bonde hilo mara baada ya kumaliza kuvuna mazao yao.

Amesema hatua hizo zitasaidia kwa kiasi kikubwa kurejesha hali ya uoto wa asili ulioharibiwa kwa kiasi kikubwa na shughuli mbalimbali za kibinadamu.

Makamu wa Rais Mhe Samia Suluhu Hassan amesisitiza kuwa sheria zote zinazohusiana na usimamizi endelevu wa ikolojia na mazingira ya Bonde la Mto Ruaha Mkuu ikiwemo sheria ya mazingira na nyingine zitekelezwe kwa ukamilifu na kila mhusika.

Amesema kuwa ili kutekeleza maagizo hayo ni vyema wadau wote wa mazingira washirikiane kikamilifu na kuwashirikisha wananchi wa maeneo husika ili wajione nao ni sehemu ya mkakati wa kuokoa mfumo wa ikolojia wa bonde hilo kwa ajili ya ustawi wa maisha yao na maslahi ya Taifa kwa ujumla.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira January Makamba amesema kikosi kazi hicho ambacho kilizinduliwa rasmi na Makamu wa Rais Mhe Samia Suluhu Hassan tarehe 11 April 2017 mjini Iringa kimefanya kazi kubwa kwa siku 30.

Amesema unauhakika taarifa ya kikosi kazi hicho ikifanyiwa kazi ipasavyo italeta mabadiliko makubwa katika Uhifadhi wa Ikolojia katika Bonde la Mto Ruaha Mkuu na kurejesha hali yake ya awali.

Waziri Makamba amesema kazi kama hiyo itafanyika katika maeneo mbalimbali nchi ili kuhakikisha uharibifu kwenye mabonde yote nchini inakomeshwa.

Ameeleza kuwa jitihada hizo zilizochukuliwa na ofisi yake tayari zimewavutia baadhi ya wahisani ambao tayari wameonyesha nia ya kushirikiana na Serikali katika Uhifadhi wa mazingira nchini.

Baadhi ya Mawaziri ambao wamepewa nafasi ya kuzungumza katika mkutano huo watatekeleza haraka iwezekanavyo maelekezo ya Makamu wa Rais ili kukomesha uharibifu mkubwa wa mazingira katika Bonde la Mto Ruaha Mkuu.


Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Post a Comment